Thursday 11 June 2015

Mimba za utotoni, nani wa kumfunga paka kengele?

 
Na Lilian Timbuka
Kwa ufupi
Hiyo ni changamoto inayolikabili taifa, huku baadhi ya watu wakiliona kuwa ni jambo la kawaida na hulipuuza wakati wengine wanalikemea.

Kila kukicha kumekuwa na kesi za migogoro ya ardhi, mirathi na hata kesi za wazazi kuozesha mabinti zao wakiwa na umri mdogo licha ya suala hilo kupigiwa kelele muda mrefu.
Hiyo ni changamoto inayolikabili taifa, huku baadhi ya watu wakiliona kuwa ni jambo la kawaida na hulipuuza wakati wengine wanalikemea.
Kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Haki za Binadamu Duniani(Amnesty) iliyozinduliwa jijini Dar es Salaam hivi karibuni, Tanzania ni moja ya nchi zinaoongoza kwa matukio ya mimba za utotoni.
Takwimu zinaonyesha kuwa, kwa siku, watoto 16 wanapachikwa mimba za utotoni.
Kwa mujibu wa wataalamu, hali hiyo imekuwa ikiendelea kwa muda mrefu na kwa asilimia kubwa inazorotesha maendeleo ya mtoto wa kike.
Ili kumwokoa mtoto wa kike kutoka janga hilo, jitihada mbalimbali zimefanywa na mashirika yasiyo ya kiserikali kuhakikisha inawaokoa hasa wale ambao tayari wameshatumbukia katika dimbwi hilo.
Utafiti uliofanywa hivi karibuni na Chama chaWaandishi wa Habari Wanawake (Tamwa), unaonyesha kuwa katika kipindi cha mwaka 2012/2013, matukio 228 ya mimba na matukio 42 ya ndoa za utotoni yaliripotiwa.
Hata hivyo, mimba na ndoa za utotoni zimetajwa kuwa miongoni mwa vikwazo vinavyowapata watoto wa kike wa Tanzania, tatizo ambalo bado ni kubwa katika baadhi ya maeneo ya Tanzania Bara na Visiwani.
Mimba za utotoni na ukatili
Kwa kiasi kikubwa tatizo hilo linakwenda sanjari na ukatili wa kijinsia ambapo kwa Tanzania Visiwani hali hiyo imeonekana zaidi katika Mkoa wa Kusini Pemba na Wilaya ya Kati Unguja, huku upande wa Tanzania Bara maeneo yenye ukatili dhidi ya wanawake pamoja na mimba za utotoni yakitajwa kuwa ni Wilaya za Kahama, Tarime, Sengerema, Newala, Mbulu, Bunda, Nkasi, Babati, Chunya, Dodoma, Bariadi, Busega na Singida vijijini.
Bokhe Odhiambo (31), mkazi wa Tarime mkoani Mara, anasema kuwa vitendo vya ukatilli dhidi ya wanawake ndani ya ndoa na mimba za utotoni kwa watoto wa kike ni mambo ya kawaida na jamii inaonekana kuwa haina muda wa kuyakemea.
“Kupigwa au kufanyiwa vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake ndani ya ndoa, migogoro ya ardhi na mimba za utotoni kwa watoto wa kike ni mambo ya kawaida tu kwenye jamii yetu licha ya wasaidizi wa kisheria kutoa elimu,” anssema Odhiambo.
Kutokana na changamoto hiyo, Chama cha Wanasheria Wanawake Tanzania (Tawla) kimejitosa kutoa msaada wa kisheria katika mikoa yenye changamoto lengo likiwa ni kupunguza tatizo hilo.
Mwenyekiti wa Tawla, Aisha Bade anasema kutokana na ukubwa wa tatizo hilo chama chake kimeamua kusambaza wasaidizi wa kisheria 400 nchi nzima lengo likiwa ni kusaidia kutatua migogoro ya ardhi na mirathi.
Bade anasema Tawla imebaini kuwa mikoa ya Pwani na Morogoro, Mtwara, Lindi, Arusha , Tanga, Shinyanga, Manyara na Mwaza inaongoza kwa kuwa na migogoro ya mirathi, vitendo vya ukatili na kuozesha watoto katika ndoa za utotoni.
Anasema kuwa mbali na mikoa hiyo pia mikoa ya Tanga, Arusha, Dodoma inaongoza kwa kuwa na migogoro ya ardhi pamoja na mirathi na hivyo juhudi mbalimbali zinahitajika kukabiliana na tatizo hilo. “Tumesambaza wasaidizi wa kisheria 400 nchi nzima lengo ni kutatua migogoro iliyopo hasa katika maeneo ya vijijini ambayo tumeona hayana msaada wa kisheria” anasema Bade.
“Mbali na mikoa hiyo pia mikoa ya Tanga, Arusha, Dodoma nayo ni miongoni mwa mikoa inayoongoza kwa kuwa na changamoto kubwa ya migogoro ya ardhi na miradhi na kwamba juhudi za pamoja zinahitajika kushirikia katika kutatua changamoto hiyo ili kupunguza madhara yanayoweza kutokea kutokana na tatizo hilo”anasema Beda.
Tawla imefanya nini?
Anasema kuwa Tawla ilianza mafunzo ya wasaidizi wa sheria mwaka 2006 na kutokana mafunzo hayo zaidi ya wananchi 4,600 wamenufaika kwa kupata msaada wa kisheria vijijini katika kipindi cha mwaka jana pekee.
John Maziku, mkazi wa mkoani Shinyanga, anasema kuwa utoro kwa wanafunzi a shule za sekondari na msingi ni tatizo linaloukabili mkoa huo kwa sasa na sababu kubwa ni wazazi kutokuwa karibu na watoto wao.
“Wazazi wengi wanakwenda migodini wanakaa huko kwa muda mrefu na hwakumbuki kama wana familia, mama anabakia na mzigo mkubwa wa kuitunza.
“Wazazi ndiyo chanzo kikubwa cha utoro katika wilaya ya Bukombe kwa sababu baba anapokwenda kwenye machimbo ya migodi hakumbuki kuwa wanaacha shule na kwenda kutafuta pesa,”anasema.
Mwajuma Mohamed (15), mkazi wa Ushirombo amekatiza masomo yake akiwa darasa la sita baada ya kupewa mimba na dereva wa magari makubwa. Hivi sasa ana mtoto wa miezi saba, lakini baba yake hajawahi kupeleka huduma ya mtoto.
Mchango wa Tamwa
Mkurugenzi Mtendaji wa Tamwa, Valerie Msoka anasema wamefanya kampeni ya kutoa elimu kwa wanafunzi wa shule za sekondai na msingi juu ya umuhimu wa elimu na madhara ya mimba za utotoni ambayo bado chama hicho kinaendelea nayo, lengo likiwa kuifikia mikoa yote nchini.
Anasema kwamba elimu hiyo imetolewa katika wilaya kumi za mikoa ya kusini ambayo ni Lindi na Mtwara na kwamba mikoa ya Pwani na Dar es Salaam imepata elimu hiyo kupitia mradi wa GEWE, unaofadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Denmark (Danida).
“Elimu inayotolewa kwa wanafunzi inalenga kumwezesha mwanafunzi namna ya kujitambua na kujua malengo ya elimu aipatayo itamsaidiaje katika maisha yake ,” anasema Msoka.
Anasema mafunzo hayo ni kitu cha muhimu na yatachangia maendeleo ya mwanafunzi hapo baadaye.
“Hata kama wazazi wanapomlazimisha kuolewa, binti anatakiwa kukataa ili aweze kumaliza elimu yake vizuri,” anasema Msoka na kuongeza: “Kazi hii ya kupambana na janga hili ni lazima pia lifanywe na wanasiasa hasa katika kipindi hiki tunachoelekea katika Uchaguzi Mkuu.” Anabainisha kuwa miongoni mwa wanasiasa imejengeka tabia ya kutotilia maanani matatizo kama ya unyanyasaji wa kijinsia, hasa kipindi kama hiki wakihofia kukosa kura.
“Ninawasihi wanasiasa, waache tabia ya kufumbia macho matatizo yanayowakabili wapiga kura wao bali wayatafutie ufumbuzi,” anasema Msoka.
Hata hivyo, swali linalobaki ni nani wa kulaumiwa kwa mimba za utotoni; ni nani wa kuwafichua watuhumiwa na kukomesha ouvu huo, nani wa kumfunga paka kengele?
                                                        Habari hii imepatikana katika gazeti la Mwanannchi.

WILAYA YA LUDEWA YAANDAA MPANGO WA KUKUZA SEKTA YA ELIMU

                                   Bw.Haji Mnasi ofisa elimu shule za msingi wilaya ya Ludewa

 Bw.Haji Mnasi ofisa elimu shule za msingi wilaya ya Ludewa akiongea na mwandishi wa habari Bw.Bazil Makungu

                                                 hii ni baadhi ya nyumba ya mwalimu 
                              Deo Filikunjombe akiongea na watendaji wa Srikali wilayani Ludewa
Mwalimu Kayombo wa shule ya msingi Masi mavalafu  mwenye shati nyeupe akitoa malalamiko ya makato ya kodi ya nyumba za walimu kwa katibu wa ccm wilaya ya Ludewa Bw.Lusiano Mbosa
 Diwani wa kata ya Ibumi Bw.Haule mwenye suti akimkabidhi zawadi ya mbunga mbunge wa jimbo la  Ludewa Deo Filiknjombe katika kijiji cha Masi mavalafu
 Filikunjombe akiongea na wananchi wa Masi mavalafu kuhusiana na shida wanazozipata walimu na utatuzi wake


Halmashauri ya wilaya ya Ludewa katika mkoa wa Njombe kupitia Idara ya elimu imeandaa mpango mkakati wa kukuza kiwango cha elimu katika ufaulu ili kushindana na wilaya zingine katika mkoa huu kwani wilaya ya Ludewa imekuwa na kiwango cha chini kwa miaka mingi na kusababisha baadhi ya wananchi kuiona idara ya elimu haifanyi kazi kwa kiwango kinachoridhisha.

Akiongea na wanahabari ofisini kwake ofisa elimu shule za msingi wilaya ya Ludewa Bw.Haji Mnasi alisema kuwa wilaya ya Ludewa imekuwa na matokeo mabaya kwa muda wa miaka mingi kutokana na changamoto mbalimbali hivyo ofisi yake kupitia wataalamu wa elimu umeandaliwa mpango mkakati utakao ivusha elimu kutoka kiwango cha hali ya chini na kuongeza ufaulu kama wilaya nyingine mkoa wa Njombe.

Bw.Mnasi alisema kuwa wilaya ya Ludewa ni wilaya kama nyingine nchini hivyo hakuna sababu ya kila mwaka kushika nafasi za mwisho kimkoa na kitaifa katika ufaulu wa wanafunzi kwani idara yake imeshazibaini changamoto zinazosababisha kutokea kwa hali hiyo na tayari suruhisho limepatikana la kukomesha hali hiyo.

Alisema kuwa mpango ulioandaliwa ni pamoja na kufanya ukaguzi wa mara kwa mara katika shule zote kupitia idara ya ukaguzi na kuhakikisha kila shule inakuwa na walimu wakutosha kwani awali kuna baadhi ya shule zilikuwa na walimu wengi na nyingine zilikuwa na hali mbaya zaidi kutokana na kuwa na mwalimu mmoja hivyo zilishindwa kutoa elimu nzuri hali iliyopelekea kutofaulisha wanafunzi.

“Idara ya ukaguzi imekuwa na hali ngumu ya kifedha hivyo ilipelekea kushindwa kufanya kazi yao vizuri lakini hata mimi mwenyewe nitapita vijijini na kuzitembelea shule mara kwa mara  ili kuleta ufanisi wa kielimu licha ya kuwa mazingira ya Ludewa ni magumu kutokana na vijiji kuwa mbalimbali hivyo inatulazimu kutumia gharama nyingi katika ufuatiliaji lakini naamini tutafanikiwa tu”,alisema Bw.Mnasi.

Bw.Mnasi alisema kuwa wilaya ya Ludewa kuna baadhi ya kata hazifikiki kwa kutumia usafiri wa gari hasa kata za mwambao wa ziwa Nyasa hivyo hulazimika kutumia boti ambayo inagharimu fedha nyingi hasa katika ununuzi wa petroli lita 200 kwa safari moja na kutokana na bajeti ya Serikali kuwa ndogo katika ufuatiliaji kwa namana hiyo ukaguzi ulifanyika zaidi kata za jirani kutokana na ufinyu wa bajeti.

Kuhusu baadhi ya walimu wapya kukataa kufanya kazi katika baadhi ya maeneo kutokana na ugumu wa mazingira Bw.Mnasi alisema kuwa halmashauri inaandaa mipango ya kutoa motisha kwa baadhi ya walimu wanaofanya kazi katika mazingira magumu ili kuinusuru elimu wilayani hapa ambapo miaka ya nyuma wilaya ya Ludewa ilisifika kwa kutoa wasomi wazuri ambao walisoma katika mazingira hayo na walimu waliweza kuishi popote bila malalamiko.

Bw.Mnasi alisema kuwa Serikali imeshawaleta walimu wapya 42 katika wilaya ya ludewa na tayari wameshaanza kuripoti wilayani hapa lakini mpango wa idara ya elimu kwa mwaka huu ni kuwasambaza walimu hao katika tarafa ya Masasi na Mwambao ambako ndiko kunauhaba mkubwa wa walimu kwa miaka mingi licha ya kuwa wanafunzi wanaotoka maeneo hayo wamekuwa na uwezo mkubwa kielimu kwa kuwatumia walimu wachache waliokuwa nao.

Wilaya ya Ludewa imekuwa na changamoto kubwa katika idara ya Elimu kutokana na halamshauri ya wilaya hii kupitisha sheria ya kuwakata fedha za malipo ya Nyumba wanazoishi walimu hata kama nyumba hiyo ni mbovu huko vijijini kila mwalimu anakatwa kiasi cha shilingi elfu kumi kwa mwezi hali ambayo imekuwa ni kero kwa walimu hao na kuwafanya kukata tamaa ya utendaji katika maeneo yao ya kazi.

Kutokana na hali hiyo inayowakumba walimu mbunge wa jimbo la Ludewa Mh.Deo Filikunjombe ameitaka Halmashauri kutengua sheria hiyo ili kuwapatia unafuu wa maisha walimu hao kutokana na ugumu wa maisha unaowakabili kwani halmashauri inaweza kubuni vyanzo vingine vya mapato na si kuwakamua walimu ambao ilipaswa wapate motisha katika kazi yao.

Mh.Filikunjombe aliyasema hayo katika kijiji cha ibumi ambako alikutana na changamoto hiyo kwani baadhi ya walimu walimweleza kuwa Serikali ya halmashauri inawapuuza na kuwanyonya kwa kuwatoza nyumba zisizo na kiwango cha kuishi walimu kwani nyumba nyingi wanazoishi vijijini hazina sakafu wala mifuniko ya madirisha hali ambayo ni hatari kwa walimu.

Mh.Filikunjombe alisema kuwa kimsingi Halmashauri inapaswa kutoa motisha kwa walimu hao kwani wengi wao wanaishi mbali na makao makuu ya wilaya hali ambayo huwalazimu wakati wa mwisho wa mwezi kutumia robo ya mshahara wao katika usafiri wanapofuata mishahara wilayani hali ambayo si kweli.

Mbunge huyo alisema kuwa anaandaa mpango wa kukutana na walimu wote wa wilaya ya Ludewa ili kuweza kuzungumza nao na kumshawishi mkurugenzi wa halmashauri kuwarudishia fedha zao wale waliokatwa kimakosa kwani kunabaadhi ya walimu vijana wanaishi watatu hadi wanne katika nyumba moja lakini kila mmoja anakatwa kiasi cha shilingi elfu kumi kwa mwezi.

Mwisho.

                                              Habari na: Habari Ludewa Blog.

  MANGULA ATAJA VIGEZO 13 VYA MGOMBEA URAIS WA CCM..NI HIVI HAPA

MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Philip Mangula amesema vigezo 13, vitatumika kuwachuja wanachama wa chama hicho ambao wameomba kugombea urais CCM.

Alisema hayo jana mjini hapa wakati wa mkutano wake na waandishi wa habari kwenye makao makuu ya CCM mjini Dodoma.

Aliwakumbusha watangaza nia kuwa hawaruhusiwi kutoa rushwa, kushawishi au kushawishika kuwapa rushwa wale wanaowadhamini.

Vigezo vyenyewe
Alitaja vigezo 13 vitakavyotumika kuwachuja wagombea kuwa ni uwezo mkubwa na uzoefu katika uongozi, uadilifu, unyenyekevu na busara.

Pia, kuwa na elimu ya chuo kikuu au inayolingana na hiyo, mtu mwenye upeo mkubwa wa kuimarisha na kuendeleza Muungano, umoja na amani.

“Anatakiwa kuwa na upeo mkubwa usiotiliwa mashaka kuhusu masuala ya kimataifa, asiye na hulka ya kidikteta au mfashisti, awe tayari kulinda kanuni, sheria na utawala bora,” alisema Mangula.

Alitaja vigezo vingine ni kuwa mtetezi wa wanyonge na haki za binadamu na asiwe na tamaa ya kujipatia umaarufu, kuzifahamu, kuzitetea, kutekeleza sera na Ilani ya CCM, mpenda haki na ajue kupambana na dhuluma, asiwe mtu anayetumia nafasi ya uongozi kujilimbikizia mali.

“Awe ni mtu makini anayezingatia masuala ya uongozi,” alisema.

Alisema katika kipindi hiki cha mchakato wa uteuzi, kanuni zitakazotumika ni zile Kanuni za Uteuzi wa Wagombea katika Vyombo vya Dola, zilizotolewa na Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM ya mwaka 2010.

Pia, katika kipindi hiki cha mchakato wa uteuzi wa wagombea wa CCM katika vyombo vya dola, ni sehemu ya kazi za chama ndani ya chama. Alisema vikao vya uchujaji, vitazingatia pia Kanuni za Uongozi na Maadili Toleo la mwaka 2012.

Alisema kipindi ambacho CCM hudhihirisha dhana ya kazi ya msingi na muhimu katika kujenga uongozi mmoja katika chama, kazi ya kutekeleza kwa dhati kanuni na demokrasia na nidhamu ndani ya chama.

Alisema kanuni hiyo, ndiyo inakiwezesha chama hicho kuwa cha demokrasia na papo hapo kuwa chombo cha kuongoza mapinduzi kutokana na nidhamu yake inayokipa uongozi moja katika vitendo.

Alisema miiko ya shughuli za uchujaji na uteuzi wa wagombea, itazingatiwa. maadili na nidhamu ya chama katika kusimamia na kutekeleza shughuli za uteuzi wa wagombea wa CCM katika vyombo vya dola, lazima vizingate na wale wote wanaohusika.

“Ni mwiko kwa kiongozi yeyote kwa maneno au vitendo kumpendelea au kumsaidia kupata kura nyingi mwombaji mmoja dhidi ya mwingine.”

Alisema Chama kinakataza mgombea kutumia au kuhusisha ukabila, dini, rushwa, rangi, hila na eneo analotoka katika shughuli yoyote ya uchaguzi.

Alisema ni mwiko kwa mgombea kufanya kampeni ya kupakana matope na ya aina nyingine yoyote ile dhidi ya mgombea mwingine.

Aidha, alisema ni mwiko kwa kiongozi yeyote au mwombaji yeyote wa nafasi ya uongozi, aliyekabidhiwa dhamana ya usimamizi, uangalizi, uchujaji na uteuzi, kufanya vitendo vya ukiukaji wa kanuni ambazo ni Katiba ya CCM, sheria, ratiba na taratibu za uteuzi.

Mangula alisema kwa mujibu wa kanuni za uteuzi wa wagombea wa CCM katika vyombo vya dola, kutangaza nia kunaruhusiwa kwa masharti, ikiwemo bila kuathiri haki ya mwanachama ya kutangaza nia wakati wowote nia yake ya kutaka kugombea nafasi fulani ya uongozi katika vyombo vya dola, lakini kwa kuwa nafasi hizo zimewekwa muda maalumu wa miaka mitano.

Alisema wakati wa kutafuta wadhamini 450, kila anachokifanya mwana CCM anayetafuta wadhamini, kitaingia katika kumbukumbu za tathmini ya mgombea mtarajiwa.

Pia, alisema kamati za maadili za wilaya, zikutane mara baada ya wagombea watarajiwa kujaza majina ya wadhamini wilayani. Alisema mpaka sasa wagombea urais waliojiandikisha wamefikia 22 na wengine bado wanakwenda.
HABARI NA MASAMA BLOG

WEKA MAONI YAKO HAPA