Wednesday 8 July 2015

MAKAMU WA KWANZA WA RAIS ZANZIBAR, MAALIM SEIF AITEMBELEA FAMILA YENYE WATOTO SITA WENYE ULEMAVU


Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, akiwa pamoja na familia ya Bw. Saleh Juma Saleh (mwenye mtoto), yenye watoto sita wenye ulemavu wa aina tofauti, huko nyumbani kwao Kinyasini Mkarafuuni Wilaya ya Wete. (Picha na OMKR)

                                                                                Na: Hassan Hamad, OMKR

Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, leo ameitembelea na kuifariji familia ya Bw. Saleh Juma Saleh yenye watoto sita wenye ulemavu.

Akizungumza na familia hiyo nyumbani kwao Kinyasini Mkarafuuni Wilaya ya Wete Pemba, katika mfululizo wa ziara yake ya kutembelea wagonjwa katika Mkoa wa Kaskazini Pemba, Maalim Seif ameitaka kuwa na subra na upendo kwa watoto hao wakielewa kuwa huo ni mtihani kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Amemuagiza Mkuu Mkuu wa Wilaya ya Wete kukutana na familia hiyo, ili kuandaa mipango itakayoweza kuwasaidia katika kuendesha maisha yao na shughuli zao za kila siku.

Baba mzazi wa watoto hao Bw. Saleh Juma Saleh amesema watoto wake wanashindwa kusoma kutokana na kukosa nyenzo kwa vile wote sita hawawezi kutembea.
Amesema watoto hao wakiwemo wanne wa kike na wawili wa kiume wanasikia vizuri, wanazungumza na wanafahamu wanachoambiwa, ingawaje baadhi ya wakati wanapoteza uelewa kutokana na hali ya ulemavu wao.
Amefahamisha kuwa iwapo watapatiwa nyenzo wataweza kwenda skuli na kusoma kama wenzao wengine, na kuiomba serikali na wasamaria wema kuwapatia misaada inayostahiki, ili nao waweze kwenda skuli.
                                              Habari na: http://rweyunga.blogspot.com/