Thursday 11 June 2015

  MANGULA ATAJA VIGEZO 13 VYA MGOMBEA URAIS WA CCM..NI HIVI HAPA

MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Philip Mangula amesema vigezo 13, vitatumika kuwachuja wanachama wa chama hicho ambao wameomba kugombea urais CCM.

Alisema hayo jana mjini hapa wakati wa mkutano wake na waandishi wa habari kwenye makao makuu ya CCM mjini Dodoma.

Aliwakumbusha watangaza nia kuwa hawaruhusiwi kutoa rushwa, kushawishi au kushawishika kuwapa rushwa wale wanaowadhamini.

Vigezo vyenyewe
Alitaja vigezo 13 vitakavyotumika kuwachuja wagombea kuwa ni uwezo mkubwa na uzoefu katika uongozi, uadilifu, unyenyekevu na busara.

Pia, kuwa na elimu ya chuo kikuu au inayolingana na hiyo, mtu mwenye upeo mkubwa wa kuimarisha na kuendeleza Muungano, umoja na amani.

“Anatakiwa kuwa na upeo mkubwa usiotiliwa mashaka kuhusu masuala ya kimataifa, asiye na hulka ya kidikteta au mfashisti, awe tayari kulinda kanuni, sheria na utawala bora,” alisema Mangula.

Alitaja vigezo vingine ni kuwa mtetezi wa wanyonge na haki za binadamu na asiwe na tamaa ya kujipatia umaarufu, kuzifahamu, kuzitetea, kutekeleza sera na Ilani ya CCM, mpenda haki na ajue kupambana na dhuluma, asiwe mtu anayetumia nafasi ya uongozi kujilimbikizia mali.

“Awe ni mtu makini anayezingatia masuala ya uongozi,” alisema.

Alisema katika kipindi hiki cha mchakato wa uteuzi, kanuni zitakazotumika ni zile Kanuni za Uteuzi wa Wagombea katika Vyombo vya Dola, zilizotolewa na Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM ya mwaka 2010.

Pia, katika kipindi hiki cha mchakato wa uteuzi wa wagombea wa CCM katika vyombo vya dola, ni sehemu ya kazi za chama ndani ya chama. Alisema vikao vya uchujaji, vitazingatia pia Kanuni za Uongozi na Maadili Toleo la mwaka 2012.

Alisema kipindi ambacho CCM hudhihirisha dhana ya kazi ya msingi na muhimu katika kujenga uongozi mmoja katika chama, kazi ya kutekeleza kwa dhati kanuni na demokrasia na nidhamu ndani ya chama.

Alisema kanuni hiyo, ndiyo inakiwezesha chama hicho kuwa cha demokrasia na papo hapo kuwa chombo cha kuongoza mapinduzi kutokana na nidhamu yake inayokipa uongozi moja katika vitendo.

Alisema miiko ya shughuli za uchujaji na uteuzi wa wagombea, itazingatiwa. maadili na nidhamu ya chama katika kusimamia na kutekeleza shughuli za uteuzi wa wagombea wa CCM katika vyombo vya dola, lazima vizingate na wale wote wanaohusika.

“Ni mwiko kwa kiongozi yeyote kwa maneno au vitendo kumpendelea au kumsaidia kupata kura nyingi mwombaji mmoja dhidi ya mwingine.”

Alisema Chama kinakataza mgombea kutumia au kuhusisha ukabila, dini, rushwa, rangi, hila na eneo analotoka katika shughuli yoyote ya uchaguzi.

Alisema ni mwiko kwa mgombea kufanya kampeni ya kupakana matope na ya aina nyingine yoyote ile dhidi ya mgombea mwingine.

Aidha, alisema ni mwiko kwa kiongozi yeyote au mwombaji yeyote wa nafasi ya uongozi, aliyekabidhiwa dhamana ya usimamizi, uangalizi, uchujaji na uteuzi, kufanya vitendo vya ukiukaji wa kanuni ambazo ni Katiba ya CCM, sheria, ratiba na taratibu za uteuzi.

Mangula alisema kwa mujibu wa kanuni za uteuzi wa wagombea wa CCM katika vyombo vya dola, kutangaza nia kunaruhusiwa kwa masharti, ikiwemo bila kuathiri haki ya mwanachama ya kutangaza nia wakati wowote nia yake ya kutaka kugombea nafasi fulani ya uongozi katika vyombo vya dola, lakini kwa kuwa nafasi hizo zimewekwa muda maalumu wa miaka mitano.

Alisema wakati wa kutafuta wadhamini 450, kila anachokifanya mwana CCM anayetafuta wadhamini, kitaingia katika kumbukumbu za tathmini ya mgombea mtarajiwa.

Pia, alisema kamati za maadili za wilaya, zikutane mara baada ya wagombea watarajiwa kujaza majina ya wadhamini wilayani. Alisema mpaka sasa wagombea urais waliojiandikisha wamefikia 22 na wengine bado wanakwenda.
HABARI NA MASAMA BLOG

WEKA MAONI YAKO HAPA

No comments:

Post a Comment