Thursday 13 August 2015

Wizara yakanusha kuwepo ebola nchini

Thursday, August 13, 2015
Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dr. Seif
Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dr. Seif Rashid. 
By Elizabeth Edward
Dar es Salaam.Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imefafanua kuwa hakuna uthibitisho kwamba mkimbizi aliyekufa kwenye kambi ya Nyarugusu mkoani Kigoma, alikuwa akiumwa ugonjwa wa ebola.
Serikali ilitoa taarifa kwa vyombo vya habari jana baada ya kuzuka hali ya sintofahamu kufuatia kifo cha mkimbizi huyo kuhusishwa na ugonjwa wa ebola ulioua maelfu wa watu katika baadhi ya nchi za Afrika Magharibi.
Agosti 9 mwaka huu, Buchumi Joel (39) akitokea katika kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu alipokelewa katika hospitali ya Mkoa wa Kigoma ya Maweni akiwa na dalili za kutokwa na damu sehemu mbalimbali za mwili, hasusan kwenye fizi, macho na masikio.
Licha ya kupatiwa matibabu ya hali ya juu kunusuru maisha yake, Buchumi aliaga dunia siku iliyofuata na kuzikwa chini ya uangalizi wa ofisi ya afya ya mkoa.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na wizara hiyo mpaka sasa hakuna uthibitisho kwamba mgonjwa huyo amekufa kutokana na ebola, licha ya kuwa na viashiria vya ugonjwa huo.
“Ili kupata uhakika wa hilo tayari sampuli ya mgonjwa huyu imechukuliwa na kupelekwa kwenye maabara ya Taifa ya Afya ya Jamii kwa uchunguzi zaidi, kujua chanzo cha ugonjwa huu,” ilisema taarifa hiyo.
Wizara hiyo imeeleza kuwa imejiandaa vyema kudhibiti ugonjwa huo iwapo utaingia nchini ikiwa ni pamoja na kutengeneza mpango kazi wa miaka mitatu kuanzia 2015 hadi 2017.
Katika hatua nyingine, wananchi wametakiwa kuendelea kuchukua tahadhari za kujikinga na ugonjwa huo uliotikisa dunia katika miaka ya hivi karibuni.
Miongoni mwa tahadhari hizo ni kuepuka kugusa au kuingiwa na mate, damu, haja ndogo, jasho, kinyesi, machozi na majimaji mengine yanayotoka mwilini mwa mgonjwa mwenye dalili za ebola kupitia sehemu zenye michubuko au vidonda.
Kutoa taarifa mapema kwa viongozi wa Serikali na kuwahi katika vituo vya kutolea huduma za afya anapohisiwa kuwepo mtu mwenye dalili za ugonjwa huo.
Mpaka sasa zaidi ya watu 11,269 wamepoteza maisha katika nchi za Guinea, Liberia na Siera Leone tangu kuibuka kwa mlipuko wa ugonjwa huo.
Jinsi ya kujikinga na ebola
-Kunawa mikono kabla na baada ya kula.
-Kusafisha mikono muda wote ili kuepuka kusambaza ugonjwa ikiwa mtu atakuwa amemshika mgonjwa au mazingira yenye maambukizi.
-Kuwahi katika vituo vya huduma za afya mtu anapohisiwa kuwa na dalili za ebola. huu.
Kuepukana na mila na desturi zinazoweza kuchelewesha kupata huduma muhimu na kuzidi kueneza ugonjwa wa ebola.
Kutumia kemikali za kuua vijidudu kutakasa mikono.
Kuepuka kushughulikia maiti ya mtu aliyekufa akiwa na dalili za ugonjwa wa ebola, badala taarifa za kifo hicho zipelekwe kwa uongozi wa kituo cha kutoa huduma za afya kwa ushauri.
                                     Habari kutoka:http://www.mwananchi.co.tz

No comments:

Post a Comment